Jumatano, 22 Safar 1448 | 2026/08/05
Saa hii ni: (M.M.T)
Menu
Main menu
Main menu

بسم الله الرحمن الرحيم

Jibu la Swali

Vita vya Amerika na Iran na Uhalisia wa Iran

(Imetafsiriwa)

Swali:

Mashambulizi ya Marekani dhidi ya Iran na majibu ya Iran kwa mashambulizi hayo yameendelea kwa zaidi ya miezi mitatu. ("Amri ya Marekani ilisema kwamba ilifanya mashambulizi ya usahihi yakilenga kambi ya amri ya kijeshi ya ardhini ya Iran kwenye Kisiwa cha Qeshm. Katika kujibu, Walinzi wa Mapinduzi ya Iran walitangaza kwamba walilenga kambi ya Marekani katika eneo hilo." (Al Jazeera, 3/6/2026)). Vile vile, mashambulizi ya umbile la Kiyahudi kusini mwa Lebanon yanaendelea. ("Mapigano yaliendelea usiku kucha kati ya "Israel" na Hezbollah kusini mwa Lebanon, licha ya tangazo la Trump kwamba pande zote mbili zilikubaliana kukomesha uhasama kabla ya raundi mpya ya mazungumzo kati ya Lebanon na "Israel", yaliyopangwa kufanyika leo jijini Washington." (BBC, 2/6/2026)). Mnamo 28/2/2026, Amerika, pamoja na mtoto wake, umbile la Kiyahudi, ilianzisha uvamizi dhidi ya Iran ambao ulidumu kwa takriban siku 40, na kuwaua takriban maafisa 40 wakuu wa kisiasa na kijeshi, akiwemo Kiongozi wake Mkuu, Ali Khamenei. Mpango ulikuwa ni kuipindua serikali au kuibadilisha kutoka dola ya satelaiti hadi dola ya tiifu. Hata hivyo, hili halikutokea. Hili lilifuatiwa na mazungumzo yasiyo ya moja kwa moja nchini Pakistan kati ya Iran na Amerika, yaliyojaa mapendekezo kutoka pande zote mbili, mvutano kati ya Marekani na mtoto wake, umbile la Kiyahudi, na majibu ya Iran. Hakuna makubaliano ambayo yamefikiwa kuhusu pendekezo lolote. Kwa hivyo, msimamo wa sasa wa Iran ni upi? Je, imekuwa dola huru, inabaki kuwa dola ya satelaiti, au inayumbayumba kati ya hizo mbili? Jazakum Allah Khair.

Jibu:

Ili kujibu maswali hapo juu, tunahakiki mambo yafuatayo:

1- Wakati Amerika, pamoja na umbile la Kiyahudi, ilipoanzisha uvamizi dhidi ya Iran mnamo 28/2/2026 na kuwaua takriban viongozi wake 40 wa kisiasa na kijeshi, akiwemo Kiongozi wake Mkuu Ali Khamenei, ambaye ni afisa mkuu zaidi nchini, kitendo hiki kinaonyesha kwamba Amerika hairidhiki na uongozi wa Iran na sera zake, na inataka kuondoa uongozi huu na kubadilisha sera hizi, kwa sababu iligundua kuwa uongozi huu una mwelekeo wa kujitegemea. Kwa hivyo, ilitaka kuleta viongozi ambao wangekuwa watiifu kwake. Kujibu swali la tarehe 4/4/2026, lenye kichwa "Vita dhidi ya Iran," tulisema: (Inaonekana kwamba hesabu za Amerika na umbile la Kiyahudi zilikuwa na dosari. Walipoanzisha uvamizi wao dhidi ya Iran, waliweka muda mfupi wa vita, unaokadiriwa kuwa siku nne, huku shambulizi kubwa na la haraka likiwalenga viongozi wake wakuu, vituo vya nyuklia, na viwanda vya makombora na maeneo ya kurusha makombora. Walidhani kwamba mara tu watakapopiga kichwa cha utawala na viongozi wake wakuu, ngazi ya pili ingejisalimisha na kukubali masharti yao, kama ilivyotokea Venezuela wakati vikosi vya Marekani vilipomteka nyara rais wake, na makamu wake wa rais na msafara wake walijisalimisha kwa Amerika. Hata hivyo, hili halikutokea Iran baada ya kuuawa kwa Kiongozi wake Mkuu, Ali Khamenei, na baadhi ya viongozi wa utawala huo. Walinzi wa Mapinduzi walisimama kidete na kuamua kukabiliana na uvamizi huu na kuwashambulia maadui…Hii inaonyesha kwamba Amerika ililenga kubadilisha sera ya utawala kutoka dola ya satelaiti hadi dola tegemezi, hivyo kuiwezesha kuamuru masharti katika mazungumzo na Iran. Hata hivyo, ilishindwa kufanikisha hili na kuamua kuendelea na vita). Hali ya sasa nchini Iran ni ile ya mgawanyiko kamili na Amerika, isipokuwa mawasiliano ya simu kati ya maafisa katika wizara za kigeni za nchi zote mbili na mawasiliano yasiyo ya moja kwa moja kupitia mtu wa tatu, kama vile Pakistan.

2- Jibu la Iran lilikuwa na athari kubwa, kwani ilikataa kurudi nyuma au kufanya makubaliano kuhusu suala la nyuklia au Mlango-Bahari wa Hormuz. "Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ilisema kwamba jibu lake lilitaka kukomeshwa kwa vita katika pande zote, ikiwemo Lebanon, kuondolewa kwa kizuizi cha majini cha Marekani kwenye bandari za Iran, na kuachiliwa kwa mali zilizoshikwa za Iran nje ya nchi chini ya vikwazo vilivyowekwa miaka iliyopita." (Al-Arabiya, 12/5/2026). Yote haya yanaonyesha kwamba mbinu zinazotumiwa na utawala wa Marekani kuamiliana na Iran na kuibadilisha kuwa dola tiifu zimefeli, na kusababisha maafisa wa Marekani kupendekeza mbinu ya uvumilivu zaidi kwa suala la Iran.

3- Trump aliposhindwa kufikia lengo lake lililotajwa kuhusu Iran kupitia vita vya siku 40 na kuuawa kwa viongozi kadhaa wa ngazi ya juu, alitangaza mpango wa nukta 15. Ni wazi kutokana na mambo ya mpango huu kwamba ni mpango wa kujisalimisha! Unalenga kuinyang'anya Iran uwezo wake wa asili, wa makombora pamoja na nyuklia. Hii ilisababisha majibu makali kutoka kwa Walinzi wa Mapinduzi, ambao walikataa kusalimu masharti ya Trump. Iran ilipokataa kujisalimisha na kusisitiza msimamo wake na utayari wake wa kupigana, Amerika ilitangaza kuanza tena kwa mazungumzo ili kusaini makubaliano nayo. Kisha ilimtuma afisa wake wa pili wa ngazi ya juu, Makamu wa Rais Vance, kwenda Pakistan kujadiliana na Wairan mnamo 11/4/2026. Vance alisema, "Yeye [Trump] hataki kufanya, kama, mpango mdogo. Anataka kufanya makubaliano makubwa...Marekani haikuwahi kuwa na mikutano katika ngazi hiyo na serikali ya Iran kwa miaka 49...Nchini Pakistan, tulipata maendeleo mengi...Mtu anayeendesha nchi hiyo nchini Iran akiwa ameketi mbele ya Makamu wa Rais wa Marekani, hilo halijawahi kutokea" (Fox News, 14/4/2026). Inaonekana kwamba rais wa Marekani alikuwa na hamu ya kupata mengi zaidi alipoona Iran ikikubali baadhi ya masharti yake, kama naibu wake alivyosema, "Hiyo ndiyo aina ya makubaliano makubwa ya Trump ambayo Rais ameweka mezani."

4- Kisha Trump alitangaza kuongezwa kwa muda usiojulikana kwa makubaliano ya kusitisha mapigano na Iran, saa chache tu kabla ya makubaliano ya kusitisha mapigano aliyotangaza kama wiki mbili zilizopita kuisha. [Urefushaji muda huu, kulingana na Trump, ulikusudiwa kuwezesha nchi zote mbili kuendelea na mazungumzo ya amani (Al Jazeera, 22/4/2026)]. Hata hivyo, Iran ilikataa kujadiliana chini ya shinikizo, ikidai kuondolewa kwa kizuizi cha Marekani kwenye bandari zake. Mnamo 20/4/2026, Trump aliandika kwenye jukwaa lake la Truth Social, "Operesheni Midnight Hammer (vita yake ya 2025 pamoja na Mayahudi) ilikuwa uharibifu kamili wa maeneo ya vumbi la nyuklia (maana yake urani iliyorutubishwa) nchini Iran. Kwa hivyo, kuichimba itakuwa mchakato mrefu na mgumu." Hili lilikuwa jaribio la kupunguza matakwa yake kwamba Iran ikabidhi urani iliyorutubishwa kwake au mtu wa tatu. Sasa anaonekana kupendelea zaidi kufikia malengo ya nchi yake kupitia mazungumzo, kwani anaamini kuyafikia kupitia vita si rahisi, kwa hivyo kubadilika katika misimamo yake. Hili linafafanua ulainishaji msimamo wake. Kusitishwa kwa mapigano hakuna wakati, na kutoa takriban kilo 441 za urani iliyorutubishwa hadi 60% kunaonekana kuwa vigumu.

5- Mnamo 13/4/2026, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Abbas Araqchi alifichua kwenye jukwaa la X maelezo ya mazungumzo na Marekani nchini Pakistan, ambapo alikuwa sehemu ya ujumbe wa nchi yake. Alisema, "Lakini tulipokuwa umbali wa shubiri chache tu kutoka kwa 'MoU ya Islamabad', tulikutana na ubinafsi, kuhama kwa nguzo za malengo, na vizuizi." Hii inalingana na kauli ya Makamu wa Rais wa Trump kwamba mambo yalikuwa karibu na makubaliano fulani, lakini Trump alitaka zaidi! Anataka Iran isalimu amri na kuwa dola tiifu kama nchi zengine katika eneo hilo. Aliongeza, "kuna mapigano makubwa na mkanganyiko ndani ya 'uongozi' wao...Ikiwa wanataka kuzungumza, wanachotakiwa kufanya ni kupiga simu!!!" (Fox News, 25/4/2026).

6- Iran inaelewa haja ya Amerika kupunguza mvutano bila vita kamili, kutokana na hali ya ndani ya Trump (kisiasa) na uwezekano wa kupoteza chama chake katika uchaguzi wa bunge wa katikati ya muhula wa Novemba. Kushindwa katika uchaguzi huo kungeathiri vibaya urais wake, kwani anahitaji idhini ya bunge kuhusu masuala mengi, ikiwa ni pamoja na kupigana vita, na pia kungeathiri nafasi zake katika uchaguzi wa rais miaka miwili baadaye. Zaidi ya hayo, Trump anafahamu kuhusu Amerika kuwa mwandalizi wa Kombe la Dunia, litakaloanza tarehe 11/6/2026. Kwa hivyo, Iran imeimarisha msimamo wake na kutangaza utayari wake wa kupigana vita tena dhidi ya Amerika na mtoto wake, umbile la Kiyahudi. Hii inaonyesha kwamba kundi ndani ya utawala wa Iran (Walinzi wa Mapinduzi) sasa linafanya kazi kwa utashi na uamuzi wake, likitafuta uhuru kutoka kwa Amerika, tofauti na kundi la kisiasa, ambalo linatamani kushirikiana na Amerika na kufanya kazi nayo kama dola ya satelaiti, angalau, badala ya dola la tiifu.

7- Trump alitumia mbinu nyingine kuishinikiza Iran. Alitangaza mnamo 4/5/2026, operesheni inayoitwa "Project Freedom" kwa kisingizio cha kusaidia meli kutoka nchi alizozielezea kuwa zisizoegemea upande wowote na zisizohusiana na mgogoro wa Mashariki ya Kati kupita katika Mlango-Bahari wa Hormuz. Hili lilipofeli, alisimamisha operesheni hiyo. Asubuhi ya tarehe 6/5/2026, alitangaza kwenye jukwaa lake la Truth Social kusimamishwa kwa operesheni hiyo, akisema, “Kulingana na ombi la Pakistan na Nchi zengine, Mafanikio makubwa ya Kijeshi ambayo tumepata wakati wa Kampeni dhidi ya Nchi ya Iran na, zaidi ya hayo, ukweli kwamba Maendeleo Makubwa yamepatikana kuelekea Mkataba Kamili na wa Mwisho na Wawakilishi wa Iran, tumekubaliana kwa pande zote kwamba, ingawa Kizuizi kitabaki kutekelezwa, ‘Project Freedom’ itasitishwa kwa muda mfupi kuona iwapo Makubaliano hayo yatakamilishwa na kutiwa saini au la.”

8- Mnamo 6/5/2026, tovuti ya habari ya Marekani Axios ilinukuu chanzo kimoja cha Pakistan kikisema, "Ikulu ya White House inaamini inakaribia kufikia makubaliano na Iran kuhusu mkataba wa makubaliano wa ukurasa mmoja ili kukomesha vita... makubaliano hayo yangehusisha Iran kukubali kusitisha utajiri wa nyuklia, Marekani kukubali kuondoa vikwazo vyake na kutoa mabilioni ya fedha za Iran zilizozuiwa, na pande zote mbili kuondoa vikwazo vinavyozunguka usafiri kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz." Hii inathibitisha kwamba Trump ana haraka ya kufikia makubaliano na Iran kwa sababu kuanza tena kwa uhasama kunahitaji idhini ya bunge, ambayo haihakikishiwi, na kwa sababu kuanza tena kwa uhasama pia haitabiriki, kwani tayari amejaribu na kushindwa. Vile vile, mradi wake wa kuokoa meli zilizokwama katika Ghuba, katika Operesheni Freedom, utachukua muda mrefu kufanikiwa na umejaa hatari, kwani Iran inatishia kulipiza kisasi, ikihatarisha meli inazotarajia kuokoa. Ni muhimu kukumbuka kwamba Trump, tajiri wa mali isiyohamishika, anataka kufikia mikataba ya kisiasa ya haraka na yenye faida, akizichukulia siasa kama muamala wa kibiashara!

9- [Rais wa Marekani Donald Trump alitangaza mnamo Jumapili kukataa kwake jibu lililowasilishwa na Iran kupitia mpatanishi wa Pakistan kuhusu pendekezo lake la kukomesha vita katika eneo hilo. Trump aliandika katika chapisho kwenye jukwaa lake la Truth Social, "Nimesoma tu jibu kutoka kwa wanaoitwa 'Wawakilishi' wa Iran. Sikupenda - HAIKUBALIKI KABISA!" Katika maoni ya kwanza kuhusu kukataa kwa Trump jibu la Iran, televisheni ya Iran ilisema, "Jibu la Tehran kwa pendekezo la Marekani la kukomesha vita, ambalo Trump alilielezea kuwa halikubaliki, lilijumuisha uthibitisho wa haki za msingi za watu wa Iran." Televisheni ya Iran iliongeza kuwa Tehran ilikataa pendekezo la Marekani kwa sababu kukubali itakuwa sawa na kujisalimisha. Ilibainisha kuwa jibu la Iran pia lilisisitiza haja ya Marekani kulipa fidia kwa vita hivyo na kuthibitisha uhuru wa Iran juu ya Mlango-Bahari wa Hormuz] (Al-Araby Al-Jadeed, 11/5/2026).

10- Jibu hili lilimkasirisha Rais wa Marekani Trump, ambaye alisema mnamo 12/5/2026: "Kusitishwa kwa mapigano ni kwa msaada mkubwa wa maisha, ambapo daktari anaingia na kusema, bwana, mpendwa wako ana takriban nafasi ya 1% ya kuishi…Wanafikiri kwamba, nitachoka na hili, au nitaboeka, au nitapata shinikizo fulani.” Aliongeza, "Kipande hicho cha takataka (jibu la Iran) walilotutumia, hata sikumaliza kukisoma..." (Al-Sharq Al-Awsat, 12/5/2026). Hata hivyo, baadaye aliongeza: "Tutaona kitakachotokea, wanataka kufanya makubaliano, wanataka kujadiliana...hatutaruhusu Iran kuwa na silaha ya nyuklia..." (Al Jazeera, 12/5/2026).

11- Kisha wakarudi kujadili marekebisho au maboresho ya makubaliano. Tovuti ya habari ya Axios, kama ilivyoripotiwa na Al-Najah News mnamo 24/5/2026, ilimnukuu afisa mmoja wa Marekani akisema [kwamba Marekani na Iran zilikuwa karibu kusaini makubaliano ya kuongeza muda wa kusitisha mapigano kwa siku 60, ambapo Mlango wa Hormuz utafunguliwa tena. Mkataba huo pia ulieleza kwamba Iran itaweza kuuza mafuta kwa uhuru na kufanya mazungumzo kuhusu kupunguza mpango wake wa nyuklia. Mlango wa Hormuz ungekuwa wazi wakati wa kipindi cha siku 60 bila ushuru, na Iran ingekubali kuondoa migodi iliyoiweka kwenye mlango huo ili kuruhusu meli kupita kwa uhuru. Ripoti hiyo iliongeza kuwa, kwa malipo, na kama sehemu ya makubaliano yaliyopendekezwa, Marekani itaondoa kizuizi chake kwenye bandari za Iran na kutoa baadhi ya vikwazo ili kuruhusu Iran kuuza mafuta kwa uhuru. Ripoti hiyo ilisema kwamba rasimu ya makubaliano pia ilijumuisha ahadi kutoka Iran za kutofuata silaha za nyuklia na kujadili kusimamishwa kwa mpango wake wa kurutubisha urani na kuondolewa kwa akiba yake ya urani iliyotajirishwa sana. Ripoti ya Axios pia ilisema kwamba Marekani itakubali kujadili kuhusu kuondolewa kwa vikwazo na kuziachilia mali za Iran katika kipindi cha siku 60. Ikulu ya White House bado haijajibu ripoti hiyo...].

12- Al Arabiya iliripoti mnamo 29/5/2026, ikinukuu Reuters, [kwamba Marekani na Iran zimefikia makubaliano ya kuongeza muda wa kusitisha mapigano, kuruhusu kuondolewa kwa vikwazo vya usafiri kupitia Mlango-Bahari wa Hormuz, kukomesha kizuizi cha Marekani cha bandari za Iran, na kuondoa baadhi ya vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Iran. Hata hivyo, makubaliano hayo bado hayajakamilika. Kufikia makubaliano kutakuwa hatua kubwa kuelekea kukomesha vita ambavyo vimeisukuma dunia katika mgogoro wa nishati, lakini kutokubaliana kimsingi kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran kutajadiliwa tu katika mazungumzo katika wiki zijazo. Makamu wa Rais wa Trump, Vance, alisema mnamo Alhamisi, "Hatujafika bado, lakini tuko karibu sana na tutaendelea kufanya kazi." Iran bado haijatoa maoni rasmi. Hata hivyo, shirika la habari la Iran lililo nusu rasmi Tasnim lilinukuu chanzo kimoja kilicho karibu na timu ya mazungumzo kikisema kwamba maandishi ya makubaliano bado hayajakamilika au kuthibitishwa. Ilichukua miaka mingi ya mazungumzo kati ya timu kubwa za wajuzi na wataalamu kufikia makubaliano kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran mwaka wa 2015. Trump alijiondoa kutoka kwa makubaliano haya wakati wa muhula wake wa kwanza wa uraisi mnamo 2018” (Al Arabiya, 29/5/2026).

13- [Ikulu ya White House ilisema kwamba Rais Trump hangekamilisha makubaliano na Tehran isipokuwa masharti yote yatimizwe. Axios ilimnukuu afisa mmoja wa utawala wa Marekani akisema kwamba kutangaza makubaliano na Iran kunaweza kuchukua siku kadhaa au zaidi ya wiki moja hadi Rais Trump apate anachotaka. Kulingana na tovuti hiyo, mashaka ya Trump yanajumuisha mambo kadhaa anayotaka yarekebishwe katika makubaliano hayo, kama vile: kufungua Mlango-Bahari wa Hormuz, Marekani kupata urani iliyorutubishwa, na marekebisho ya rasimu ya mpango wa nyuklia wa Iran. Gazeti la New York Times liliripoti kwamba marekebisho mapya ya Trump, yaliyojadiliwa na ushiriki wa wapatanishi wa Pakistan, yalirudishwa Tehran ili yazingatiwe na uongozi wa Iran. Yalionyesha kwamba kuchelewa zaidi kwa tangazo rasmi la makubaliano hayo kunatarajiwa kutokana na ugumu wa mawasiliano ya moja kwa moja na Kiongozi Mkuu wa Iran Mojtaba Khamenei. Wakati huo huo, Kamandi Kuu ya Marekani (CENTCOM) inaendelea kuimarisha kizuizi chake cha majini kwenye bandari za Iran (Al Jazeera, 31/5/2026)].

14- Wakati huo huo, huku makubaliano kati ya Trump na Iran yakiendelea kubadilika, umbile la Kiyahudi linaendelea na uvamizi wake dhidi ya kusini mwa Lebanon:

A- [Jeshi la ‘Israel’ lilisema kwamba liliteka Ngome ya Beaufort kufuatia mapigano makali yanayosaidiwa na mizinga mikubwa na ulinzi wa anga, sanjari na ongezeko kubwa lililojumuisha maeneo ya Nabatieh, Wadi al-Salouqi, na Wadi al-Hujeir. Kuongezeka huku kwa ghasia kulitokea katika muktadha wa mapambano na Hezbollah nchini Lebanon katika muktadha wa mzozo wa Marekani-‘Israel’-Iran mwishoni mwa Februari 2026 (Al Jazeera, 1/6/2026)].

B- [Jeshi la ‘Israel’ lilitoa onyo la kuhamishwa kwa wakaazi wa vitongoji vya kusini mwa Beirut saa chache baada ya Waziri Mkuu Netanyahu kutangaza maagizo ya kuongezeka mashambulizi ya kijeshi. Katika taarifa iliyotolewa Jumatatu alasiri, jeshi la Israel lilisema kwamba ikiwa Hezbollah itaendelea kufyatua makombora katika miji na vijiji vya ‘Israel’, litajibu kwa kushambulia shabaha katika vitongoji vya kusini mwa Beirut (Al Jazeera, 1/6/2026)].

C- Ingawa Al-Arabiya Net ilichapisha mnamo 2/6/2026, kwamba Rais wa Marekani Trump (aliashiria katika simu kwamba tatizo dogo limetokea, lakini alisisitiza kwamba alilishughulikia haraka sana, akielezea kwamba lilihusiana na kutoridhika kwa Iran na mashambulizi ya Israel dhidi ya Lebanon, akiongeza, "Kwa hivyo, nilizungumza na Hezbollah, na nikasema hakuna ufyatuaji risasi, na nikazungumza na 'Bibi' (Netanyahu), na kusema, hakuna ufyatuaji risasi, na wote wawili wakaacha kufyatuliana risasi" (Al-Arabiya.net, 2/6/2026), umbile la Kiyahudi halikulichukua hili kumaanisha Lebanon yote, bali kwa vitongoji vya kusini mwa Beirut pekee, na liliendelea na uvamizi wake dhidi ya kusini, kama kawaida kwa idhini kutoka kwa Trump, ambaye haliwezi kumuasi, na kuendelea na mashambulizi yake dhidi ya kusini mwa Lebanon:

[Chini ya kichwa cha habari: msimamo wetu hautabadilika katika 'Israel', Netanyahu alisema kwamba alimwambia Trump kwamba vikosi vyake vitashambulia Beirut ikiwa Hezbollah haitaacha kushambulia 'Israel'. Aliongeza, kulingana na taarifa iliyotolewa na afisi yake, "Msimamo wetu bado haujabadilika." Wakati huo huo, jeshi litaendelea kufanya kazi kama ilivyopangwa kusini mwa Lebanon” (Arabia Huru, 2/6/2026)]. [Mapigano yaliendelea usiku kucha kati ya “Israel” na Hezbollah kusini mwa Lebanon licha ya Trump kukandamiza maasi ya ndani, Kiongozi Mkuu mpya anawategemea kudumisha utawala wake. Ingawa mfumo wa kisiasa bado upo Iran, ikiwa ni pamoja na Rais, Waziri wa Mambo ya Nje, na Spika wa Bunge, na ingawa lengo lao kuu ni Iran kurudi kwenye mzunguko wa Marekani, ushawishi wao halisi hauwezi kusimama dhidi ya Walinzi wa Mapinduzi.

15- Nukta zifuatazo zinaibuka kutokana na mfululizo huu wa matukio na matokeo yake:

A- Mzozo bado unaendelea kati ya Iran na Amerika, na kwa sasa hakuna uratibu kati yao wa kufanya kazi pamoja katika eneo hilo kama dola ya satelaiti, kama ilivyokuwa hapo awali. Hii ni kweli hasa ikizingatiwa kwamba Walinzi wa Mapinduzi sasa wanadhibiti serikali nchini Iran, na wanasukuma uhuru, ikimaanisha kukataa kurudi kwenye mzunguko wa Marekani. Inawezekana kwamba wataendelea kudhibiti serikali, kwani walikuwa muhimu katika kumchagua Kiongozi Mkuu mpya, Mojtaba. Zaidi ya hayo, katika masuala muhimu ya utawala, kama vile vita na kukandamiza maasi ya ndani, Kiongozi Mkuu mpya anawategemea kudumisha utawala wake. Ingawa mfumo wa kisiasa bado upo Iran, ikiwa ni pamoja na Rais, Waziri wa Mambo ya Nje, na Spika wa Bunge, na ingawa lengo lao kuu ni Iran kurudi kwenye mzunguko wa Marekani, ushawishi wao halisi hauwezi kusimama dhidi ya Walinzi wa Mapinduzi.

B- Kinyume chake, Amerika hadi sasa imeshindwa kuifanya serikali nchini Iran iwe chini yake, kama tawala zengine za vibaraka katika nchi za Kiislamu. Licha ya haya, Trump anasisitiza kwamba serikali nchini Iran iwe chini yake, si kuzunguka duara lake la ushawishi kama ilivyokuwa hapo awali, licha ya kushindwa kwake katika juhudi hii. Anataka kila kitu kutoka Iran, ikimaanisha 100% ya matakwa yake, sio 90% au 95% kama asemavyo: “Sitaki 90%,  sitaki 95%. Nimewaambia nataka kila kitu...” (TV Lebanon, 12/4/2026). Na ni leo tu, Jumatano, 3/6/2026, anasema: “(Hali ya Iran) inabadilika kwa haraka na inabadilika vizuri,” akiashiria kuwa Iran imekubali kutomiliki silaha za nyuklia… (Al Arabiya, 3/6/2026). Huku kauli za Trump sio zote zikiwa sahihi, hii ndio misimamo yake aliyoitangaza: kwamba Trump anataka Iran iwe dola kibaraka ambayo haimpingi, licha ya kufeli kwake kufikia hili! Ili kuficha kufeli huku, anatumia maneno, anakariri rasimu ya makubaliano, kisha anarudi kuyapinga… na kadhalika!

C- Lakini kitakachovunja mgongo wa Trump na (kina Trump) wengine miongoni mwa wakoloni makafiri kama yeye, kwa sababu tu ya kufikiria uchokozi dhidi ya ardhi za Waislamu, na kumrudisha kila kafiri nyumbani kwake, ikiwa bado angali na nyumba, ni kurudi kwa Khilafah Rashida. Na itarudi, Mwenyezi Mungu akipenda, ahadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu (swt):

[وَعَدَ اللَّهُ الَّذِينَ آمَنُوا مِنْكُمْ وَعَمِلُوا الصَّالِحَاتِ لَيَسْتَخْلِفَنَّهُمْ فِي الْأَرْضِ]

“Mwenyezi Mungu amewaahidi wale walio amini miongoni mwenu na wakatenda mema, ya kwamba atawafanya makhalifa katika ardhi” [An-Nur: 55], na bishara njema kutoka kwa Mtume wa Mwenyezi Mungu (saw) baada ya utawala huu dhalimu tunaoishi chini yake: Ahmad amepokea kutoka kwa Hudhayfah akisema: «... ثُمَّ تَكُونُ مُلْكاً جَبْرِيَّةً فَتَكُونُ مَا شَاءَ اللَّهُ أَنْ تَكُونَ، ثُمَّ يَرْفَعُهَا إِذَا شَاءَ أَنْ يَرْفَعَهَا، ثُمَّ تَكُونُ خِلَافَةً عَلَى مِنْهَاجِ النُّبُوَّةِ. ثُمَّ سَكَت» “... Kisha kutakuwa na utawala kandamizi (ملكًا جبرية) kwa muda anaotaka Mwenyezi Mungu, kisha atauondoa atakapo kuundoa, na kisha kutakuwepo na Khilafah kwa njia ya Utume, kisha (saw) akanyamaza.” Hivyo, kutakuwa na khalifa ambaye watu watapigana vita nyuma yake na watalindwa naye, kisha Uislamu na Waislamu watakirimiwa, na ukafiri na makafiri watadhalilishwa.

[وَيَوْمَئِذٍ يَفْرَحُ الْمُؤْمِنُونَ * بِنَصْرِ اللَّهِ يَنْصُرُ مَنْ يَشَاءُ وَهُوَ الْعَزِيزُ الرَّحِيمُ]

“Na siku hiyo Waumini watafurahi * Kwa nusura ya Mwenyezi Mungu humnusuru amtakaye. Naye ndiye Mwenye nguvu Mwenye kurehemu.” [Ar-Rum: 4-5]

17 Dhul Hijjah 1447 H

3 Juni, 2026 M

Andika maoni

Hakikisha umejaza (*) habari zinazohitajika palipoashiriwa. Kodi za HTML haziruhusiwi.

rudi juu

Vifungu vya Tovuti

Viunganishi

Magharibi

Ardhi za Waislamu

Ardhi za Waislamu